Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Thursday, May 30, 2013

MTENDAJI ALIEKULA KISIRI MILIONI 14 AZIREJESHA HADHARANI BAADA YA KUBANWA KATIKA MJI MDOGO WA TUNDUMA


Afisa mtendaji wa mtaa wa Chapwa Daniel Sinkonde aliyekula milioni 14 akisubiri kuzikabidhi pesa hizo
a
Hapa afisa huyo akiandika hati ya makabidhiano mbele ya Diwani na wananchi
Huu ni mkataba wa awali endapo angeshindwa kulipa nyumba iuzwe
Mtendaji huyo akihesabu hela anazorejesha 
Watendaji wengine wakiesabu hela hizo

Mtendaji akiomba msamaha 
Baadhi ya wananchi walioshuhudia urejeshwaji wa pesa hizo
 Diwani wa Kata ya Tunduma Frank Mwakajoka alisema baada ya kupewa taarifa hizo aliamua kufuatilia na kumbana  Mtendaji huyo kuhusu madai hayo ya Wananchi ambapo Mei 23, Mwaka huu alikiri kuhusika na kudai kuwa alipewa  Laki saba pekee ambazo alizikabidhi katika Ofisi ya Serikali ya Kijiji.



KATIKA Hali isiyo kuwa ya kawaida Wakazi wa Kitongoji cha Isanzo Mtaa wa Chapwa uliopo katika Kata na Mji mdogo wa Tunduma wilaya ya Momba Mkoani Mbeya wamefanikiwa kuzikomboa fedha zilizokuwa zimeliwa na Afisa Mtendaji wa Mtaa huo zaidi ya Shilingi Milion 14.


Tukio hilo la aina yake lilitokea hivi karibuni katika Mkutano wa hadhara  uliofanyika Chapwa katika Mji huo baada ya baadhi ya wananchi kumtuhumu Mtendaji huyo kujipatia fedha kinyume na utaratibu kutokana na malipo ya fidia ya eneo la Kitongoji cha Isanzo lililochukuliwa na Mamlaka ya mapato (TRA) kwa ajili ya ujenzi wa Nyumba za watumishi.
 

Kwa mujibu wa Wananchi waliofika katika mkutano huo uliokuwa ukiongozwa na Diwani wa kata ya Tunduma  Frank Mwakajoka(CHADEMA) walisema chanzo cha Mtendaji huyo Daniel Sinkonde kula fedha hizo ni kutokana na kufoji majina ya wakazi wa Kitongoji hicho waliokuwa wakistahili kulipwa fidia kutoka TRA.
 

Walisema wakati Mamlaka ya Mapato ilipohitaji majina ya wakazi hao kwa ajili ya kulipwa fidia, Mtendaji huyo aliamua kutunga majina sita ambayo aliyapeleka TRA ambapo Mamlaka hiyo iliandika hundi kwa wahusika ambao baada ya kukabidhiwa fedha zao walizipeleka kwa Mtendaji ambaye aliwalipa Shilingi Laki 5 kila mmoja kama kifuta jasho.
  

Waliongeza kuwa baada ya kukamilisha kwa zoezi hilo mtu mmoja kati ya Sita ambaye alijulikana kwa jina la Vasta Choka alilipwa Shilingi laki Tatu badala ya Laki Tano kama wenzie walivyolipwa ambapo alipojaribu kufuatilia alibaini kudhulumiwa ndipo suala hilo lilipotinga kwa wananchi na hatimaye kumfikia Diwani.

Waliyataja majina yaliyoghushiwa na viwango vya fedha  kwenye mabano vilivyolipwa na Mamlaka ya Mapato (TRA) kuwa ni Elisa Sinkonde (mil 3,281,680/=),John Siwakwi ( Mil 2,387,800/=), Frank Mshani ( Mil 2,740,080/=), Vasta Choka 2,542,680/=), Jumatatu Silagwe (Mil 1,279,320/=) na Ezekia Kuyokwa (Mil 1,961,400/=) na jumla yake ni Shilingi Milion 14,192,960/=.
   
Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Tunduma Frank Mwakajoka alisema baada ya kupewa taarifa hizo aliamua kufuatilia na kumbana  Mtendaji huyo kuhusu madai hayo ya Wananchi ambapo Mei 23, Mwaka huu alikiri kuhusika na kudai kuwa alipewa  Laki saba pekee ambazo alizikabidhi katika Ofisi ya Serikali ya Kijiji.

Alisema kutokana na kukiri huko pamoja na kurudisha fedha hizo alienda katika Ofisi za Mamlaka ya Mapato na kubaini kuwa Mtendaji huyo alikuwa ameshalipwa zaidi ya Milion 14 kutokana na malipo ya Fidia ya viwanja kwa majina feki yaliyopelekwa.
   
Mwakajoka aliongeza kuwa awali Mtendaji huyo aliahidi kuzilipa fedha zote na kwamba endapo angeshindwa aliweka nyumba yake kama dhamana nyumba yenye hati ya kiwanja namba KAL 521 yenye thamani ya Shilingi Milion 30.
Kutokana na kusuasua huku baadhi ya wananchi kutojua mustakabali wa Mtendaji huyo waliamua kuitisha mkutano wa Hadhara kwa lengo la kumshinikiza Mtendaji huyo kuzirejesha fedha zilizobaki ambapo alipofika Mkutanoni alikutwa na Shilingi Milion 4 tu hivyo wananchi kupandwa na hasira ya kutaka kuuza nyumba yake.
 
Baada ya kutokea kwa mtafaruku huo ndipo alipojitokeza Mfanyabiashara mmoja aliyefahamika kwa jina la Adolf Mwanyangala kumdhamini kwa kumkopesha  Milion 3 na Laki tano ambazo alilipa na kufanikisha kumaliza deni lote.
   
Aidha alipotakiwa kuzungumza lolote Mtendaji huyo aliomba msamaha na kuongeza kuwa halikuwa kusudio lake na alifanya hivyo kwa bahati mbaya tu na kuwaomba wananchi wamsamehe.

Pia wananchi walimwomba Mkurugenzi Mtendaji wa Mji mdogo wa Tunduma kumfukuza kazi kabisa Mtumishi huyo kutokana na kutokuwa na sifa za utmishi wa umma.

Picha na Ezekiel Kamanga
Mbeya yetu

2 comments:

Anonymous said...

Safi sana wananchi sasa wamekuwa na ujasiri, wametafakari na kuchukua hatua! Diwani

Anonymous said...

Hongera nyingi sanaaa kwa Diwani na wananchi wote kwa kudhibiti dhuluma,rushwa na uizi. Nawapa pongezi kw awananchi wote wa kijiji hicho cha Tunduma, kazeni mwendo huo huo msikubali kuibiwa wala kudanganywa. hongera sana. na ninashukuru kwa blog hii kutuletea habari hiii.